Serikali ya Sudan: Hatukuwa na taarifa kuhusu safari ya ujumbe wa Kizayuni Khartoum
Msemaji wa serikali ya Sudan amedai kuwa baraza la mawaziri la nchi hiyo halina taarifa kuhusu safari ya ujumbe wa Kizayuni huko Khartoum mji mkuu wa Sudan.
Faisal Mohamed Saleh Msemaji wa serikali ya Sudan amedai kuwa hakuna mawasiliano yoyote yaliyofanyika kuhusu kualikwa au kuwepo taarifa kuhusu kuwasili huko Khartoum ujumbe huo tajwa wa Israel. Duru za Kizayuni Jumatatu wiki hii ziliripoti kuwa, ujumbe mmoja wa ngazi ya juu wa utawala wa Kizayuni wa Israel umewasili Khartoum baada ya kutangazwa kufikiwa mapatano ya kuanzishwa uhusiano rasmi kati ya Sudan na Israel.
Wizara ya Mambo ya Nje ya Sudan tarehe 23 mwezi Oktoba mwaka huu ilitangaza kuwa, nchi hiyo na utawala wa Kizayuni zimefikia mapatano ya kuanzisha uhusiano wa kidiplomasia kati yazo chini ya usimamizi wa Marekani. Sudan ni nchi ya tatu kutangaza kufikia mapatano ya kuanzisha uhusiano wa kidiplomasia na Tel Aviv baada ya Imarati na Bahrain.

Wakati huo huo makundi mengi ya kisiasa ya Sudan yamepinga vikali mapatano hayo kati ya nchi hiyo na utawala wa Kizayuni.