Ugaidi wa kiuchumi unazuia nchi kadhaa kupata dawa na vifaa vya tiba
Msemaji wa Tume ya Usalama wa Taifa na Sera za Kigeni katika Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu, Bunge la Iran, amesema ugaidi wa kiuchumi unazuia nchi kadhaa duniani kupata dawa na vifaa vya kitiba.
Abolfazl Amoui, Msemaji wa Tume ya Usalama wa Taifa na Sera za Kigeni katika Bunge la Iran ameongeza kuwa: "Ugaidi wa kiuchumni umezilenga nchi kadhaa na kuzizuia kupata dawa za dharura, huduma na vifaa vya kitiba katika kukabiliana na janga la corona."
Akizungumza Alhamisi katika Kikao cha Nne cha Maspika wa Mabunge kuhusu kukabiliana na ugaidi wa kiuchumi na kuimarisha ushirikiano wa kieneo ameongeza kuwa: "Baada ya kuibuka janga la COVID-19, serikali ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ilifanya kila iwezalo kukabiliana na ugonjwa huo."
Amoui ameendelea kusema kuwa, Mohsen Fakhrizadeh, mwanasayansi maarufu wa Iran na ambaye alikuwa mstari wa mbele katika kuunda chanjo ya COVID-19 au corona, alikufa shahidi baada ya kushambuliwa katika hujuma ya kigaidi mwezi Novemba mwaka jana.

Msemaji wa Tume ya Usalama wa Taifa na Sera za Kigeni Katika Bunge la Iran aidha amesema nchi nyingi zinalaani vikali ugaidi wa kiuchumi na zinautaja ugaidi huo kuwa ni kitendo cha woga, kilicho kinyume cha sheria na cha kishetani chenye lengo la kuvuruga usalama na amani kieneo na kimataifa.
Amesema Shahidi Fakhrizadeh alikuwa na nafasi muhimu katika shughuli nyingi za utafiti katika sekta ya nyuklia kwa malengo ya amani na pia katika uga wa kitiba nchini Iran.