Sanders: Afghanistan inakabiliwa na janga kubwa
Seneta wa jimbo la Vermont nchini Marekani amezungumzia hali mbaya ya Afghanistan na kutoa wito kwa serikali ya Marekani kuachilia mabilioni ya dola fedha za Afghanistan yanayozuiliwa nchini humo.
Seneta Bernie Sanders pia ametahadharisha kuhusu mgogoro mkubwa unaoisumbua Afghanistan na kuandika katika ujumbe uliochapishwa kwenye mtandao wa Twitter kwamba: "Afghanistan inakabiliwa na janga la binadamu. Ninatoa wito kwa serikali ya Biden kuachilia mara moja mabilioni ya dola, fedha za serikali ya Afghanistan, zinazozuiliwa na serikali ya Washington."
Seneta huyo mashuhuri wa Marekani amesema: Kutolewa kwa fedha zinazozuiliwa Washington kutasaidia kuzuia mzozo na vifo vya mamilioni ya watu nchini Afghanistan.

Kusimamishwa misaada ya kigeni na hatua ya Marekani ya kuzuilia fedha za kigeni za Afghanistan baada ya kundi la Taliban kuidhiti tena nchi hiyo mwaka jana kumesababisha mgogoro na maafa makubwa nchini humo.
Hivi karibuni, Kamati ya Kimataifa ya Uokoaji ilisema katika ripoti yake kwamba ukosefu wa chakula nchini Afghanistan huenda ukaongezeka zaidi katika mwaka huu wa 2022 kutokana na uhaba wa chakula, kupanda kwa kasi kwa bei za bidhaa na ukame unaoendelea nchini humo.